Zahera kuwasilisha mapendekezo ya usajili kwa uongozi Yanga



Zahera kuwasilisha mapendekezo ya usajili kwa uongozi Yanga

Baada ya mchezo dhidi ya Ruvu Shooting, uongozi wa Yanga utakutana na kocha Mkuu wa timu hiyo Mwinyi Zahera ambapo pamoja na mambo mengine, Zahera atawasilisha mapendekezo yake ya usajili, imefahamika

Makamu Mwenyekiti wa Yanga Fredrick Mwakalebela amesema kikao hicho ni cha pili kufanyika tangu uongozi mpya uingie madarakani

Amesema kikao cha kwanza kilikuwa cha Kamati ya Utendaji ambacho kiliweka maazimio mawili, moja; kuhakikisha Yanga inashinda michezo mitatu iliyobaki na la pili linahusu usajili

"Kikao chetu kilikuwa na agenda mbili, moja ni usajili ambao tutakutana na Zahera baada ya kumaliza mchezo wetu dhidi ya Ruvu Shooting na nyingine kumaliza ligi kwa heshima," amesema

"Tulivyopewa uongozi, timu ilikuwa inaongoza katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, hivyo tumeweka mikakati kushinda mechi zote tatu zilizobaki na kujua hatima yetu huko mbele"

Katika kikao hicho inaelezwa Zahera atawasilisha majina ya wachezaji ambao ametaka waendelee kubaki Yanga ili kuanza mchakato wa kuhuisha mikataba kwa wale ambao mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu

Zahera pia atawasilisha majina ya wachezaji wapya anaotaka kuwasajili

Jumamosi ya wiki hii May 18 Yanga imeandaa tukio la futari na chakula cha jioni litakalofanyika Hoteli ya Serena jijini Dar es salaam ambapo kwenye tukio hilo itafanyika Harambee ya kuichangia Yanga

Wageni mbalimbali wanatarajiwa kualikwa katika Harambee hiyo wakiwemo wabunge, mashirika mbalimbali ya Serikali na binafsi, taasisi za dini na wadau wote wenye mapenzi na Yanga

Aidha siku hiyo Kamati ya Hamasa itakabidhi kwa uongozi kiasi cha fedha ambazo zimekusanywa tangu kuanzishwa kwa kampeni ya kuichangia Yanga


KWA TAARIFA ZA MICHEZO KILA SIKU

PAKUA APP YA MIKOGO HAPA

https://play.google.com/store/apps/details?id=com.mikogo.blog

Comments